0

Maafisa wa polisi wa Kenya wamemtia nguvuni mshukiwa anayetuhumiwa kuendesha akaunti ya Twitter ambayo ina uhusiano na kundi la kigaidi la Al shabaab na uliotoa habari kwamba Al shabaab walihusika kutekeleza mauaji eneo la Mpeketoni kaunti ya Lamu.

Kwa mujibu wa Ripota Julius Kepkoech toka Kenya, Katibu wa wizara ya Mambo ya ndani na usalama wa taifa, Mutea Iringo amethibitisha kwamba Ismail Omondi ametiwa nguvuni Tarehe 18 June mwaka huu ambapo hata hivyo Iringo amekanusha kwamba mshukiwa huyo hana uhusiano wowote na Al Shabaab.

Iringo amesema, “Unaweza kuona kwamba yule anayekiri kuhusika na Alshabaab si mmoja wa kiongozi wa kundi hilo,”.

Inspekta Jenerali wa Polisi David Kimaiyo awali alisema kupitia ukurasa wake wa Twitter kwamba: “Aliye kizuizini kwa sasa ni mshukiwa anayeendesha mtandao wa kijamii unaodhaniwa kutumiwa na Al shabaab kukiri kuhusika na uvamizi”

Hata hivyo Kimaiyo hakutoa taarifa zaidi kuhusiana na washukiwa.

Ismail Omondi ni mshukiwa wa tatu kutiwa nguvuni kuhusiana na mauaji yaliyotokea Mpeketoni siku ya Jumapili na Jumatatu ambapo zaidi ya watu 60 wamepoteza maisha.

Mapema siku ya Jumatano, mshukiwa mwingine Ahmed Abdallah anayetuhumiwa kumiliki gari lililowabeba wavamizi hao alikamatwa huku Salim Dyana naye akikamatwa na polisi kwa tuhuma za kuliendesha gari lililowabeba wavamizi kuelekea Mpeketoni Lamu.

Post a Comment

 
Top